Insha hii ni ya kujadili aidha huitwa insha ya mdahalo; mtahiniwa hupeana hoja ili kuunga mkono wazo ambalo anaona linapazwa kupewa kipaombele. Mtahini anapenda kuona kama mtahiniwa ataweza kumshawishi vya kutosha katika mdahalo wenyewe kwa kupeana mawazo mazito mazito labda katika kupinga au kuunga mkono mada kuu.
Mwanafunzi anapaswa kuandika hoja za upande mmoja asichanganyechanganye. Akiisha maliza basi anaweza kutaja machache ya mlengo huo mwingine bora tu asiandike mengi ili upande anaounga au kupinga uwe na hoja nyingi zaidi.
Mwanafunzi anapaswa pia kuhitimisha kwa kuonyesha amesimama wapi huku akiwaonyesha walioko upande wa pili katika mjadala huo sababu hasa ya kuwa katika upande alioko.
Insha hii huhitaji mwanafunzi apange vidokezi vyake kwa wakati ili aone ni upande upi ana mawazo ya kutosha. Kumbuka pia kuna uwezekano mtahini atoe mada iliyo na upande mmoja tu. Basi mtahiniwa atafute hoja za kutosha na azijadili kwa mapana na marefu.
Mfano:
Kusomea shule za bweni ni bora kuliko za kutwa. Jadili
Insha hii ina sehemu mbili:
a) Ubora wa shule za bweni au malazi– Kuunga
– Muda mrefu wa kusoma
– Muda mrefu na wakufunzi
– Hakuna kutazama runinga
– Nidhamu ni ya hali ya juu
– Ukomavu na kujitegemea
– Utangamano na wanafunzi mbalimbali
– Usawa
– Kuzuru
b) Ubora wa shule za kutwa – Kupinga
– Kuwa na wazazi wake
– Mlo bora
– Matibabu mazuri
– Wazazi kufahamu maendeleo yako
Mwanafunzi ana uhuru wa kujadili upande anaojihisi ataweza kutoa hoja za kutosha. Akiamua kuunga asimamie upande huo kwa urefu na kina. Mtindo huu wa kuunga au kupinga ama kushughulikia pande moja pakee ndio aula.
Akiamua kupinga atoe hoja na asijadili kisha mwishoni atoe hoja kidogo za upande wa kuunga.
Zipo mada za upande mmoja tazama mada ifuatayo:
Pesa ni mwanzo wa uovu, jadili. Mada hii inahitaji uonyeshe vile pesa zinavyoleta uovu pekee.
Mwanafunzi ajue kuwa mtahini ana aja ya kusikia tu vile maovu yanaletwa na pesa. Mwanafunzi achunge mno asije akaelezea wema wa pesa katika mada hii.
Tanibihi:
Mwanafunzi hasipinge wazo lake la kuunga kama ukanushi. Katika upande wa kupinga tunatoa ubora/uzuri wa upande wa pili wa mada. Mfano:
(Kuunga) Watoto wa shule za malazi wana nidhamuya hali ya juu kwa kuwa ni sharti kama ibada wao kufuata sheria.
(kupinga) Unapopinga basi usiseme: Katika upande mwingine wanafunzi wa kutwa pia wana nidhamu kwa kuwa wazazi ni wakali kama simba na wao wanawatia nidhamu kwa kuwaadhibu wanapokosa. Huku si kupinga bali ni kukosoa kwa kukanusha mawazo awali.
Kwa hivyo peana wazo jingine tofauti ambalo halipo katika upande wa kuunga.
Kwa mfano: (Kuunga) Watoto wa kutwa wana bahati kama mtende kwa kuwa wana wavyere wao kila uchao. Hali hii huwapa wazazi nafasi nzuri ya kuwajua na kuwafahamu wakembe wao.
Haki zote zimehifadhiwa @ Mdarisi Bundi Mbijiwe